Saturday, July 27, 2013

Bale aipigia magoti Spurs 
WINGA wa kimataifa wa Wales, Gareth Bale, amewaomba maofisa wa klabu yake ya Tottenham kumruhusu ajiunge na klabu ya Real Madrid ya Hispania.
Tamko la Bale limekuja saa chache baada ya miamba hiyo ya soka ya Hispania kupandisha dau la ofa yake na kufikia ada rekodi ya dunia ya pauni milioni 81, ambalo pia limeonekana kupuuzwa na Spurs.
Gazeti la Marca la nchini Hispania, ambalo liko karibu mno na vyanzo vya ndani klabuni Santiago Bernabeu, limedai kuwa Bale aligeuka mbogo kwa maofisa wa klabu yake kwa kuonesha dharau kwa donge nono.
Hasira za Bale zinatokana na Madrid kuonesha nia ya dhati ya kupata saini yake, kwa dau linalovunja rekodi iliyowekwa na Cristiano Ronaldo alipoihama Manchester United kujiunga na Madrid, Julai 2009.
Bale, 24, anaamini kuwa kunahitajika kukosa uelewa kwa Mwenyekiti wa Spurs, Daniel Levy na klabu yake kukataa dau kubwa kama hilo kwa ajili yake.
Gazeti la Marca limedai kuwa, Bale amevunja ukimya na kumwambia Mwenyekiti wake Levy: “Kumbuka ulichoniahidi. Uliniahidi kuwa kama Spurs haitofuzu michuano ya Ligi ya Mabingwa Ulaya na kisha kukaja ofa nzuri utakuwa tayari kuisikiliza.
“Naam, hatimaye ofa rekodi ya dunia imewasili na kimsingi nataka kuichezea Real Madrid. Hivyo unapaswa kutoa ridhaa na kuingia katika mazungumzo ya makubaliano,” amekaririwa Bale akimwambia mwenyekiti huyo wa Spurs.
Bale alikutana na Levy na kuweka wazi kutoona mwanga katika matarajio yake klabuni hapo na imetabiriwa kuwa dau nono zaidi ya hapo linaweza kuvunjika mahusiano ya winga huyo na Bodi ya Spurs kama wataendelea kumbania.
Masikini Taifa Stars Yakosa 
tiketi ya CHAN mwaka 2014 
Kiungo Mtanzania, Amir Kiemba alipambana ndani ya Uwanja
wa Taifa wa Mandela. (Picha kwa hisani ya IssaMichuzi BLOG)
TIMU ya soka ya Tanzania, Taifa Stars inaweza kufananishwa na sikio la kufa ambalo kamwe huwa halisikii dawa, licha ya juhudi kubwa za kusaka tiba.
Ndivyo ilivyo kwa timu hiyo ambayo baada ya Juni 8 kupoteza nafasi ya kucheza fainali za Kombe la Dunia nchini Brazil, jana imeshindwa tena kupata tikjeti ya fainali za Afrika kwa nyota wa Ligi za Ndani-CHAN.
Kwa kipigo cha siku hiyo cha mabao 4-2 kutoka kwa Ivory Coast kwenye Uwanja wa Taifa jijini Dar es Salaam, kikafuta hesabu za
Brazil, hivyo turufu pekee ilikuwa ni fainali za CHAN nchini Afrika Kusini, pia za mwakani.
Katika mechi ya jana iliyochezwa kwenye Uwanja wa Taifa wa Mandela, mjini Namboole, nje kidogo ya Kampala, Stars wakiwa nyuma kwa bao 1-0 walilofungwa Julai 13, jijini Dar es Salaam, walifungwa tena 3-1.
Kwa idadi mabao 4-1, sio tu imeitupa Stars nje ya vita hiyo ya kwenda Brazil na kuipa Uganda tiketi ya Afrika Kusini, pia imetoa jawabu kwamba kazi kubwa inahitajika ili kuwa na timu bora. 
Stars iliyocheza fainali za kwanza nchini Ivory Coast mwaka 2009 chini ya Mbrazil Marcio Maximo, ilimaliza kipindi cha kwanza kwa sare ya bao 1-1.
Wenyeji walioanza kufunga bao dakika ya saba katika mechi iliyochezeshwa na Kanoso Abdoul Ohabee kutoka Madagascar, likifungwa na Frank Kalanda akimalizia mpira uliopigwa ndani ya eneo la hatari la Stars.
Bao hilo liliwafanya Stars watulie zaidi na kufanikiwa kusawazisha dakika ya 18, mfungaji akiwa Amri Kiemba kutokana na pasi nzuri ya Mrisho Ngasa kwenye kona ya eneo la mita 18.
Dakika ya 32 nusura Stars ipate bao, lakini mkwaju maridadi wa Ngasa ambao tayari ulikuwa umempira kipa Hamza Muwonge, uligonga mwamba kabla ya kuokolewa na mabeki.
Mabao la pili la wenyeji katika mechi hiyo lilifungwa dakika ya 48, Brian Majwega kabla ya Kalanda kuongeza la tatu dakika ya 63, kutokana na makosa ya Salum Abubakar kupokwa mpira akiwa kwenye nafasi nzuri ya kutoa pasi kwa mwenzake.
Kocha Kim Poulsen alifanya mabadiliko dakika ya 43, akimwingiza Simon Msuva badala ya Frank Domayo aliyeumia na dakika ya 78 akawaingiza kwa mpigo Haruna Chanongo na Vincent Barnabas na kuwatoa David Luhende na John Bocco.
Hata hivyo mabadiliko hayo hayakubadili matokeo ya mchezo ambapo hadi mwisho, wenyeji Uganda waliibuka na suhindi wa mabao 3-1, hivyo kujitwalia tiketi ya Afrika Kusini kwa jumnla ya mabao 4-1.
Kikosi cha Stars kilipangwa hivi; Juma Kaseja, Erasto Nyoni, David Luhende/Vincent Barnabas, Aggrey Morris, Kelvin Yondani, Athuman Idd, Frank Domayo/Simon Msuva, Salum Abubakar, John Bocco/Haruni Chanongo, Amri Kiemba na Mrisho Ngasa.
Stars inayodhaminiwa na Kilimanjaro Premium Lager itarejea nyumbani leo saa 4 usiku kwa ndege ya PrecisionAir. 
Demba Ba namuogopa Rooney Chelsea
MSHAMBULIAJI, Demba Ba, amekana taarifa kuwa anajiandaa kutimka klabuni Stamford Bridge, kukimbia ujio wa Wayne Rooney kama Chelsea itafanikiwa kupata saini ya nyota huyo wa kimataifa wa England.
Badala yake, Ba nyota wa kimataifa wa Senegal amemkaribisha kwa mikono miwili, Rooney anayechezea Manchester United, huku akiongeza kuwa Darajani ni sehemu sahihi ya ushindani na yu tayari kwa vita ya namba.
Ba ameongeza kuwa anawakaribisha wakali zaidi wa safu ya mbele klabuni hapo, ili kuwaongezea nguvu yeye, Fernando Torres na Romelu Lukaku.
“Nadhani tunahitaji ushindani na tunawakaribisha washambuliaji na wachezaji bora katika kikosi chetu. Ushindani kikosini utanifanya mimi kuwa bora dimbani kwa kila namna.
“Bila shaka wachezaji wote wanataka kucheza, si tu washambuliaji wa kati. Lakini tutafanya kazi kwa pamoja kama timu katika huo huo, kwa manufaa na ustawi wa klabu, kujaribu na kushinda michezo. Hivyo basi, ndiyo nitabaki hapa hata akija Rooney.”
Ba alifunga moja ya mabao ya Chelsea katika ushindi wa mabao 8-1 dhidi ya Indonesia XI juzi usiku mbele ya mashabiki wapatao 65,000 na amekiri kuwa itakuwa na msisimko wa aina yake kwake kucheza msimu huu chini ya kocha mpya Jose Mourinho.
Aliongeza kuwa: “Daima inakuwa ni jambo zuri mno kufunga, lakini katika hatua hii zaidi inakuwa ni kuhusu kuwajibika na kukaza msuli ipasavyo dimbani ili kurejea hali uhatari kama ilivyokuwa huko nyuma.
“Najisikia vizuri. Imekuwa wiki nzuri kikazi chini ya kocha mpya. Tutaona mambo yatakuwaje katika wiki chache zijazo. Itakuwa hali ya kusisimua sana,” alitamba Ba
Bolt hashikiki London
BINGWA mara sita wa michuano ya Olimpiki, Usain Bolt, ameendeleza msimu kwa ushindi katika mbio za mita 100, wakati aliporejea kwa kishindo kwenye Uwanja wa Olimpiki jijini hapa katika maadhimisho ya mwaka mmoja baada ya michuano hiyo.
Juzi, katika sherehe za mwaka mmoja tangu ufunguzi wa michuano ya Olimpiki ya Kiangazi mwaka jana 2012 jijini hapa, Bolt alilipa fadhila ya ushindi wake wa dhahabu ya michuano hiyo kwenye dimba la Olimpiki kwa kukimbia akitumia sekunde 9.85.
Mwingereza James Dasaolu alijitoa kabla ya kuchuana na Bolt katika umbali huo kutokana na majeruhi yanayomkabili.
Mmarekani Michael Rodgers alikamata nafasi, huku Mjamaica mwenzake Nesta Carter akikamata nafasi ya tatu akitumia sekunde 9.99, wakati Mwingereza pekee katika mbio hizo Dwain Chambers, akimaliza wa tano kwa sekunde 10.10.
Bolt, ambaye anatarajiwa kuutetea ubingwa wa dunia wa mita 100 mwezi ujao jijini Moscow, Russia, alionekana mwenye furaha kuu kushinda mbio hizo mbele ya mashabiki 60,000.
“Ni jambo zuri la kuvutia kushiriki mashindano jijini London, ni uzoefu wa aina yake kwa mimi kuwa hapa kwa mara nyingine," alisema Bolt kwa furaha, huku akiongeza kuwa yampasa kufanya kazi kwa bidii kuelekea kutetea ubingwa wa dunia.
"Uanzaji wangu wa mbio ulikuwa mbovu na nahitaji kulifanyia kazi hilo. Ili kuwa na mbio nzuri, nahitaji kuanza vema na kumaliza kwa ushindi. Ninatumaini kuwa nitakuwa na kipindi kizuri jijini Moscow na kuendelea kufanya vema mchezoni,” alisisitiza Bolt.
Wamiliki wakana kuiuza Liverpool
KAMPUNI ya Fenway Sports Group (FSG) imezikana taarifa za vyombo vya habari zilizodai kuwa inajiandaa kuiuza klabu ya Liverpool.
Magazeti yaliripoti Ijumaa, mabilionea wawili raia wa Marekani na kampuni moja ya Saudia inayojihusisha na uuzaji wa mafuta, zimeingia katika mazungumzo ya kuinunua Liverpool kutoka kwa FSG, ambayo ilidaiwa kutaka dau la pauni milioni 350.
Kutokana na taarifa hizo, kwa pamoja FSG na Liverpool zimekanusha kwa nguvu moja habari hizo na wamiliki wa Kimarekani ambao walianza kuimiliki Liverpool tangu Oktoba 2010, walielezea nia yao ya kuendelea kubaki Anfield.
Msemaji wa Fenway Sports Group alisema: “Kama ulivyowahi kuwa uvumi mwingine wowote kuhusu kuuzwa kwa Liverpool Football Club, hakuna ukweli wowote pia katika tetesi hizi.
“Hatujawahi kuwa na mkutano na mtu yeyote kuhusu kuiuza klabu, hatujui ni nani hasa chanzo cha uvumi huo, na lolote linalohusiana na upotoshaji juu ya mauzo ya Liverpool.”
Naye msemaji wa Liverpool, akaongeza: “Fenway Sports Group imeweka wazi kila kitu Liverpool Football Club haiuzwi. Hakuna ukweli wowote katika habari hiyo.”
Brandts wa Yanga achota ujuzi Uefa 
Kocha wa Yanga, Ernie Brandts
KOCHA Mkuu wa mabingwa wa soka Tanzania Bara, Yanga, Ernie Brandts, kesho Jumatatu anatarajia kuwa mmoja wa makocha watakaohudhuria kozi ya mafunzo ya na kuongeza muda wa leseni ya Shirikisho la Soka Ulaya (Uefa) itakayofanyika nchini Ujerumani.
Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa kwenye tovuti ya klabu hiyo jana, Brandts atakuwa mmoja wa washiriki wa kozi hiyo kwa ngazi ya Daraja la Kwanza, itakayofanyika kwa siku tatu kuanzia Jumatatu Julai 29 hadi Julai 31.
Taarifa hiyo imeongeza, baada ya kozi hiyo Brandts anatarajia kurejea nchini Agosti 1, kuendelea na maandilizi
ya msimu mpya wa Ligi Kuu ya Vodacom na michuano ya klabu barani Afrika, ambako Yanga inacheza Ligi ya Mabingwa.
Brandts amekwenda kuhudhuria kozi hiyo ya Uefa, ambayo hutolewa kila baada ya miaka miwili kwa makocha wenye leseni zinazotambuliwa na shirikisho hilo kwa ajili ya kuongeza muda (uhai) wa leseni hizo.
Uongozi wa klabu ya Yanga umebariki safari ya mafunzo kwa kocha Brandts, ukiamini itamuongezea ujuzi atakoutumia kuijenga timu, ikiwamo kuipa uwezo wa kutetea ubingwa wa Ligi Kuu na kung’ara katika mashindano ya klabu Afrika.
Brandts alijiunga na Yanga mwaka jana akitokea kuinoa APR ya Rwanda, ambapo katika msimu wake wa kwanza wa Ligi Kuu ya Vodacom ameiwezesha kutwaa ubingwa uliokuwa ukishikiliwa na watani wao wa jadi, Simba.
Yanga inatarajia kucheza mechi ya Ngao ya Hisani dhidi ya Makamu Bingwa, Azam FC hapo Agosti 17 kwenye Uwanja wa Taifa kabla ya kurejea tena dimbani hapo Agosti 24 kucheza mechi ya ufunguzi wa Ligi Kuu dhidi ya Ashanti United ya Ilala iliyorejea msimu huu kutoka Lifi Daraja la Kwanza.
Mkenya azimia kwenye mbio
 Irine Chebet Cheptai
MKIMBIAJI wa mbio ndefu wa kimataifa wa Kenya, Irine Chebet Cheptai, juzi alikimbizwa hospitali kwa matibabu baada ya kupatwa na mshituko wa moyo kwenye Uwanja wa Olimpiki baada ya kumaliza mbio za mita 3,000.
Cheptai, binti wa miaka 21, alimaliza mbio akiwa nafasi ya 11, katika muda bora zaidi katika rekodi yake binafsi, alipotumia dakika 8:56.20, lakini akaanguka ghafla na kupoteza fahamu baada tu ya kuvuka mstari wa kumalizia.
Madaktari waliokuwa uwanjani hapo wakaharakisha kumtundikia mtungi wa Oksijeni, ambapo kwa mujibu wa taarifa kuhusiana na tukio hilo zilipasha kuwa alikuja kurejewa na fahamu akiwa hospitalini.
Tukio lake limeshtua wengi kutokana na kukimbia katika mbio fupi kulinganisha na zile alizozoea za mita 5,000, ambazo ameshiriki Diamond League mara mbili msimu huu, na anakumbukwa kwa rekodi yake ya dakika 14:50.99 jijini Shanghai, Mei mwaka huu.