Sunday, October 13, 2013

Neymar moto wa kuotea mbali Brazil

Neymar moto wa kuotea mbali Brazil
BRAZIL chini ya Kocha wake Luiz Felipe Scolari, jana iliichapa Korea Kusini katika mechi ya kirafiki ya kimataifa, ukiwa ni ushindi wa tatu mfululizo kabla ya kuikabili Zambia, Jumanne ijayo katika mechi nyingine ya kimataifa.
Mabao ya wenyeji hao wa fainali za Kombe la Dunia za mwakani, yalifungwa na Neymar na  Oscar.
Neymar alifunga bao lake mwanzoni mwa kipindi cha pili kwa mpira wa adhabu ya moja kwa moja na kumtungua kipa Jung Sung-Ryong kabla ya Oscar  kufunga jingine kwa shuti kali.

Ujerumani, Ubelgiji, Uswisi zatwaa tiketi

Ujerumani, Ubelgiji, Uswisi zatwaa tiketi
Ozil ndani ya nyumba

TIMU za Ujeruamni, Ubeljigi na Uswisi, juzi usiku zilijitwalia tiketi ya Kombe la Dunia za mwakani nchini Brazil kutoka bara la Ulaya ambalo litatoa jumla ya timu 12.

Wakati maimba hiyo ikitangulia, bingwa mtetezi Hispania chini ya kocha wake Vicente Del Bosque, England na Russia, zinasubiri majaaliwa yao katika mechi za mwisho, Oktoba 15.
Ujerumani imejitwalia tiketi yake baada ya juzi kuifunga  Ireland 3-0 huku Ubelgiji ikiichapa Croatia 2-1 na Uswisi kuichakaza Albania 2-1.
Miamba hiyo imeungana na mingine kama Italia na Uholanzi iliyotangulia kupata tiketi ya Brazil.
Akizungumzia mafanikio ya Ubelgiji, kiungo Marouane Fellaini alisema wanapaswa kujivunia kiwango cha timu yao kwani pamoja na ugumu wa kampeni hiyo, wamefanikiwa.
Nazo England, Hispania na Russia zilishinda na kuongoza makundi yao, japo zinasubiri kupata matokeo mazuri katika mechi hizo za mwisho.
Kinara katika makundi tisa ya Ulaya, atajitwalia tiketi ya Brazil huku nane zitakazomaliza nafasi ya pili, zitachuana hatua ya mtoano kuwania nafasi nne kufikia 12 kwa Ulaya.
Mabao ya Ujerumani yalifungwa na Sami Khedira, Andre Schuerrle na Mesut Ozil, nyota wa Arsenal ya England aliyetokea Real Madrid ya Hispania.
Ujerumani imekata tiketi ya Kombe la Dunuia ikitokea kundi C, itacheza fainali hizo mara ya 18 tangu kuasisiwa kwake mwaka 1930.
Katika mechi nyingine, bao la dakika ya 86 likifungwa na Zlatan Ibrahimovic, liliipa Sweden ushindi wa 2-1 dhidi ya Austria, ikiwa nafasi ya pili huku Faroe Islands ikitoka sare ya 1-1 dhidi ya Kazakhstan.
Wachezaji wa Ubelgiji wakishangilia baada ya kufuzu Kombe la Dunia
Mbao mawili ya Romelu Lukaku, yaliipa Ubelgiji pointi tatu hivyo kuongoza kundi A, hivyo kuikwaa tiketi ya fainali za Kombe la Dunia mara ya kwanza tangu 2002 huku  Croatia ya pili.
Nayo Wales juzi ilishinda 1-0 dhidi ya Macedonia 1-0 katika mechi nyingine ya kundi hilo.
Aidha, mabao ya Xherdan Shaqiri na Michael Lang yaliipa ushindi Uswisi na kukamata usukani wa kundi E, hivyo kujitwalia tiketi ya Brazil huku Iceland iliyoichapa Cyprus 2-0, imebaki nafasi ya pili, mbele pointi moja dhidi ya  Slovenia iliyoichapa Norway 3-0.
Nayo England, juzi ilishinda 4-1 dhidi ya Montenegro 4-1 mjini London, hivyo kuongoza kwa tofauti ya pointi moja dhidi ya Ukraine, iliyoifunga Poland 1-0 katika kundi H.
England inahitaji ushindi katika mechi ya mwisho dhidi ya Poland hapo Oktoba 15, kutwaa tiketi huku Ukraine ikimaliza na San Marino, iliyofungwa 3-0  na Moldova.
England ilitangulia kupata bao dakika ya 49, likifungwa na Wayne Rooney kabla ya Branko Boskovic wa Montenegro kujifunga, likiwa la pili kwa England.
Hata hivyo, Dejan Damjanovic aliifungia Montenegro bao, lakini bao la Andros Townsend na Daniel Sturridge, yaliipa England ushindi wa mabao 4-1.
Raha ya ushindi
Katika kundi I, mabingwa wa Dunia Hispania waliwafunga Belarus 2-1 na kukamata usukani wa kundi mbele ya Ufaransa.
Mashuti ya Xavi Hernandez na Alvaro Negredo, ndio yalipeleka kilio kwa Belarus, hivyo sasa kuhityaji walau sare tu kutoka kwa Georgia kujitwalia tiketi ya Brazil.
Nayo Russia iliitandika Luxembourg 4-0, hivyo kukamata usukani wa kundi F, mbele ya Ureno iliyotoka sare ya 1-1 dhidi ya Israel huku Azerbaijan ikishinda 2-0 dhidi ya  Ireland Kaskazini.
Bosnia-Herzegovina iliichapa Liechtenstein 4-1, huku Ugiriki ikiifunga Slovakia 1-0, hivyo kukabana katika kundi G, wakiwa na pointi 22. Lithuania imeifunga Latvia 2-0.

Mtoano
Uturuki na Romania zimejiweka kwenye mazingira ya kucheza hatua ya mtoano wa timu nane kuania nafasi nne kutokana na kufungana kwa pointi katika kundi D, mbele ya Hungary iliyochapwa 8-1 na Uholanzi.
Hiyo ni baada ya Uturuki kushinda 2-0 dhidi ya Estonia 2 huku Romania ikishinda 4-0 dhidi ya Andorra.
Timu nne za kundi B, zimebaki kupigania kucheza hatua ya mtoano baada ya Italia kuvuna sare ya 2-2 dhidi ya  Denmark.
Denmark na Bulgaria, zilizofungwa 2-1 dhidi ya Armenia, zinafungana kwa pointi 13 kila moja huku Armenia na Czech iliyoshinda 3-1 dhidi ya Malta, zikiwa na pointi 12ts.

Zenye tiketi ya Brazil
Ukimwondoa mwenye Brazil mwenye tiketi ya moja kwa moja, nyingine ni Argentina, Australia, Ubelgiji, Costa Rica, Ujerumani, Iran, Italia, Japan, Uholanzi, Korea Kusini, Uswisi na Marekani.

Simba, Yanga jinsi zilivyotoa dozi

Simba, Yanga jinsi zilivyotoa dozi
Singano 'Messi' (kushoto) akimoka mchezaji wa Prisons 

BAO la dakika ya 62, likifungwa na Jonas Mkude, jana liliiwezesha Simba kuizamisha Tanzania Prisons ya Mbeya bao 1-0 katika mechi kali iliyochezwa Uwanja wa Taifa, jijini Dar es Salaam.
Mkude alifunga bao hilo kwa ustadi mkubwa kwa shuti ya nje ya 18 na kwenda moja kwa moja kwenye nyavu za maafande wa Tanzania Prisons, ukianzia mpira wa kona iliyopigwa na Edward Christopher.
Kabla ya bao hilo, Prisons walikianza kipindi cha kwanza kwa kasi wakicheza soka ya kujiamini wakipiga pasi nyingi za uhakika na kufanya mashambulizi kadhaa, hivyo kuwapa Simba wakati mgumu.
Dakika ya 34, Simba walimtoa Omary Salum na kumwingiza Haruna Shamte kwenda kuimarisha sehemu ya kiungo kukabiliana na presha ya vijana wa Tanzania Prisons, hivyo kwa kiasi fulani yaliwasaidia kuleta uhai.
Hata hivyo, pamoja na mashambulizi kadhaa kwa kila upande, hadi mwamuzi wa mechi hiyo Simon Mbelwa kutoka Pwani anamaliza dakika 45, kulikuwa hakuna timu iliyokuwa imepata bao.
Kipindi cha pili, vijana wa Simba chini ya kocha wake Abdallah King Kibadeni Mputa, walizidi kuonesha uhai zaidi huku maafande wa Tanzania Prisons nao wakicheza soka ya kuvutia kukiwepo kosa kosa kadhaa kwa kila lango.
Baada ya Simba kupata bao katika dakika ya 62, mechi hiyo ilionekana kuchangamka zaidi kutokana na maafande wa Prisons kucharuka wakitaka kusawazisha huku Simba nao wakipambana kuokoa hatari zote.
Dakika ya 67, Simba walifanya mabadiliko kwa kumtoa Christopher aliyempisha Zahor Pazi, mabadiliko ambayo hata hivyo hayakuweza kubadili sana suara ya mchezo.
Dakika ya 89, Prisons nusura wapate bao kama si Peter Michael kupiga shuti hafifu licha ya kuunasa mpira uliokuwa umetemwa na kipa wa Simba, Abel Dhaira, nyoya wa kimataifa wa Uganda.
Hadi mwamuzi Mbelwa anamaliza mechi hiyo, Simba walitoka kifua mbele kwa bao hilo moja, hivyo kuendelea kuongoza ligi kwa pointi 18.
Simba: Abel Dhaira, Nassor Masoud Chollo, Omary Salum, Gilbert Kaze, Joseph Owino, Jonas Mkude, Ramadhani Singano, Abdulhalim Humud, Amis Tambwe, Edward Christopher na Haruna Chanongo.
Prisons: Beno David,Kimenya Mashaka, Raulian Mpalile, Nurdin Issa, Mwangama Lugano, Nimkaza Jumanne, Kwanga Julius, Jimmy Shoji, Peter Michael, Omega Semeni na Jeremiah Mgunda.
Katika mechi nyingine iliyochezwa Uwanja wa Kaitaba, mjini Bukoba, mabingwa watetezi wa ligi hiyo, Yanga walivuna ushindi wa mabao 2-1 katika iliyokuwa na ushindani mkubwa.
Kwa ushindi huo Yanga wamefikisha pointi 15, hivyo kuendelea kuipumulia Simba kwa tofauti na pointi tatu huku kila moja ikiwa imecheza mechi nane tangu kuanza kwa msimu huu.
Baada ya mechi za jana, watani hao watakwenda mafichoni kujiandaa na mechi yao ya kukata na shoka itakayochezwa Oktoba 20, kwenye Uwanja wa Taifa, jijini Dar es Salaam.
Ligi hiyo itaendelea tena leo kwa mechi ya vibonde Ashanti United ya Ilala kuikabili Coastal Union ya Tanga kwenye Uwanja wa Azam Complex, Chamazi,nje kidogo ya jijini Dar es Salaam.
Ashanti ikiwa inaburuza mkia kwa pointi zake mbili tangu kuanza kwa ligi hiyo Agosti 24, itakuwa ikipigania ushindi wa kwanza wakati Coastal Union yenye pointi 11, itakuwa ikisaka ushindi kuzidi kujiimarisha kwenye msimamo.
Nayo Ruvu Shooting ya Pwani yenye pointi 10, itakuwa mwenyeji wa Rhino Rangers kwenye Uwanja wa Mabatini, Mkoani, Pwani huku Mgambo JKT ya Tanga ikiwa mwenyeji wa Mbeya City kwenye Uwanja wa Mkwakwani, jijini Tanga.
Azam iliyo nafasi ya nne kwenye msimamo ikiwa na pointi 11, itakuwa kwenye uwanja wa Taifa, jijini Dar es Salaam kukwaruzana na JKT Ruvu ya Pwani yenye pointi 12 huku Mtibwa Sugar ikiwakaribisha JKT Oljoro kwenye Uwanja wa Manungu, Turiani, Morogoro.