Sunday, July 21, 2013

Fabregas, Ronaldo na Rooney
Fab, Rooney, Ronaldo wamtesa Moyes
MRITHI wa Sir Alex Ferguson, David Moyes, anapitia kipindi kigumu katika timu ya Manchester United kutokana na kukabiliwa na vita ya kumbakisha Wayne Rooney huku akiwatamani Cesc Fabregas wa Barcelona na Cristiano Ronaldo wa Real Madrid.
Kocha huyo yuko katikati ya shinikizo kutoka kwa Chelsea, Barcelona na Real Madrid kuwahusu nyota hao watatu.
Chelsea wameongeza presha kwa Moyes baada ya kusema wapo tayari kumtwaa Rooney
kwa dau la pauni milioni 24 huku yeye akiboresha ofa ya kumpata Fabregas hadi pauni milioni 30.
Wakati hajajua majaaliwa ya Rooney na ujio wa Fabregas Old Trafford ukiota mbawa kutokana na kung’ang’aniwa na Barcelona na yeye kusema yu tayari kubaki, Moyes amechanganyikiwa kwani hata Madrid wamesema hawana mpango wa kumtoa Ronaldo.
Carlo Ancelotti wa Real Madrid, amemwaga dharau kwa Man United juu ya mpango wao wa kumrejesha winga huyo wa Kireno Old Trafford, akisema anawaza kusaini mkataba mpya Bernabeu.
Bosi wa Chelsea, Jose Mourinho amevuta kasi ya aina yake katika jaribio la kumng’oa Rooney na kupandisha dau lake kutoka pauni milioni 20 mapema wiki jana hadi kufikia pauni milioni 24 licha ya Moyes kukana kumuuza.
Kubwaga manyanga kuinoa Barca kulikofanywa na kocha Vilanova, kunailazimisha miamba hiyo ya Nou Camp kuachana na wazo la kumuzaa Fabregas, mshindi wa Kombe la Dunia, hadi itakapojua kocha mpya na mahitaji yake kikosini.
Kutokana na kuyumba kwa jaribio la kumnasa Fabregas na kumbakisha Rooney, maelezo ya Ancelotti kuhusu Ronaldo si habari nzuri kusomwa au kusikiwa Moyes, ambaye alikuwa na matumaini makubwa akishirikiana na Fergie kupata saini ya Mreno huyo.
Ancelotti aliyerithi mikoba ya Jose Mourinho aliyetimkia Chelsea, alimmwagia sifa nyota wake huyo aliyedai kuwa anaweza kuwa msukumo kwa nyota vijana  klabuni Bernabeu.
Mtaliano huyo alisema: “Cristiano ni nyota wa daraja la juu. Ni mchezaji mkubwa. Kwa klabu hii, jambo muhimu ni kuhesabu wachezaji wakali wa kulipwa waliopo. Wachezaji vijana humuangalia bingwa katika kuhakikisha wanafanya kama yeye.
“Sio jukumu langu linapokuja suala la kumpa mkataba mpya kubaki hapa, lakini sidhani kama kunaweza kuwa na tatizo lolote katika hilo,” alimaliza kocha huyo aliyeipa ubingwa wa Ligue 1 klabu ya PSG na kutimkia Bernabeu.
Yanga yakwepa kipigo cha Simba 
Wachezaji wa Yanga wakishangilia bao la kuzawazisha dhidhi ya URA ya Uganda, lililofungwa na Jerson Tegete katika dakika ya 90 ya mchezo na kufanya matokeo kuwa 2-2. Mchezo huo wa kimataifa wa kirafiki umefanyika leo kwenye Uwanja wa Taifa jijini Dar es Salaam.
MABINGWA wa Soka Tanzania Bara, Yanga, jana almanusra wapate aibu kama ya watani wao Simba, baada ya kulazimisha sare ya mabao 2-2 kwa URA ya Uganda.
Simba, juzi ilikumbana na kichapo cha mabao 2-1 kwenye Uwanja wa Taifa jijini Dar es Salaam kutoka kwa Watoza Ushuru hao wa Uganda, mabao yote yakifungwa Litumba Yayo.
Lakini katika hali ya kushangaza, mshambuliaji anayetarajiwa kusajiliwa na Yanga, Ogbu Brendan, raia wa Nigeria, licha ya kupangwa kikosi cha kwanza, hakuonekana dimbani kwa kile kilichoelezwa kuumia, hivyo nafasi yake kuchukuliwa na Didier Kavumbagu.
Beki wa URA ya Uganda, Lutimba Yayo akimpa 'konga' Mshambuliaji
wa Yanga, Jerson Tegete huku akimiliki mpira.
Mechi hiyo ya jana iliyopigwa kwenye uwanja huo, ilianza kwa kasi na dakika ya 41, mtambo wa mabao wa URA, Litumba Yayo, ulimtungua kipa wa Yanga, Deogratius Munishi ‘Dida’.
Kama haitoshi, alikuwa ni Yayo tena dakika ya 51, aliyepachika bao la pili kwa mkwaju wa adhabu ndogo.
Yanga walifanya mabadiliko kadhaa, ambayo yalibadilisha sura ya mchezo na kufanikiwa kujipatia bao la kwanza dakika ya 66 likifungwa Kavumbagu kwa kichwa baada ya krosi ya Juma Abdul.
Ndipo dakika ya 72 alipoingia kiungo wa kimataifa Rwanda Haruna Niyonzima kwa kuchukua nafasi ya Bahanunzi, nakuanza kuubadilisha mchezo kwa ujumla huku tetesi zikisema kuwa alifika uwanjani akitokea moja kwa moja Uwanja wa ndege wa Mw.J.K. Nyerere alipowasili wakati anatokea nchini kwao Rwanda.
Wakati mashabiki wakianza kuondoka uwanjani wakiamini Yanga imelala 2-1, alikuwa ni Jerry Tegete aliyefuta aibu kwa kupachika bao la kusawazisha katika dakika za majeruhi.
Heka heka nguo kuchanika ndani ya dimba
Yanga: Deo Munishi ‘Dida’, Juma Abdul, Oscar Joshua, Ibrahim Job, Rajab Zahir, Salum Telela, Saidi Bahanuzi, Hamis Thabit, Jerry Tegete, Brendan Ogbu, Shaban Kondo.
URA: Mugabi Yastin, Derick Walulya, Sekito Samwel, Docea Mussa, Joseph Owino, Nkungwa Elkanel, Peni Ali, Lutimba Yayo, James Kasibante, Ngama Emmanuel, Bwete Brian.
URA itashuka katika dimba la Mkwakwani jijini Tanga, Jumatano kukipiga na Wagosi wa Kaya, Coastal Union.
Wachezaji wa URA wakishangilia bao la pili
Tito Vilanova
Guardiola amhurumia Vilanova
KOCHA wa Bayern Munich ya hapa, Pep Guardiola, ameelezea masikitiko aliyonayo, kutokana na changamoto ngumu itokanayo na maradhi ya kansa ya tezi iliyomlazimisha swahiba wake Tito Vilanova kubwaga manyanga kuinoa FC Barcelona.
Akizungumza baada ya taarifa ya Vilanova kujiuzulu, Guardiola alikiri kuumia moyo kiasi cha kushindwa kuzungumza lolote akiwa nje ya Hispania; jambo linalomhusu nduguye huyo aliyekuwa akimsaidia kabla ya kurithi mikoba yake.
“Ni vigumu mno kwangu kuzungumzia suala hili kwa hapa Ujerumani. Vilanova ni zaidi ya rafiki yangu wa karibu na niseme ukweli kuwa nampenda sana,” alisema Guardiola alipokuwa akihojiwa na vyombo vya habari vya Hispania.
Guardiola aliongeza: “Naweza tu kusema kwamba namtakia kila la heri yeye na familia yake katika kukabiliana na kipindi hiki kigumu. Hili ni jambo gumu sana kwangu.”
Alionekana kukwepa kuzama zaidi kuhusu Vilanova.
Wawili hao hawakuwa na mawasiliano mazuri katika siku za karibuni, baada ya kuzaliwa kwa vita ya maneno iliyoibuliwa na Guardiola, akiilalamikia bodi ya Barca kuyatumia maradhi ya Vilanova kumchafua.
Katika madai yake, Guardiola alikuwa akikana madai ya viongozi wake hao wa zamani kuwa licha ya Vilanova kufanyiwa upasuaji, Guardiola hakuwa na muda wa kumtembelea wodini alikolazwa licha ya kuishi New York alikokuwa anaugulia.
“Sitokuja kusahau kuwa wao walitumia maradhi ya Vilanova kuniathiri mimi na kunichafua, kwa sababu ilikuwa ni uongo wa dhahiri kwamba mimi sikuwahi kumtembelea hospitalini jijini New York,” alisema Guardiola.
Vita ya maneno baina ya wawili hao ikaibuka hivi karibuni, baada ya Vilanova kuwatetea mabosi wake hao kwa kusema hakuna hata mtu mmoja miongoni mwa bodi ya klabu hiyo aliyetumia maradhi yake ya kansa kumshambulia Guardiola.
Vilanova alikaririwa akisema: “Pep amefanya vibaya na kimsingi imenishangaza sana kutokana na maelezo yake. Hakuna yeyote katika bodi klabu aliyetumia maradhi yangu kumshambulia yeye kama alivyodai.
Na Vilanova akaongeza: “Guardiola alinitembelea mara moja tu toka nilipowasili jijini New York, lakini baada ya operesheni nikawa naugulia huko kwa miezi miwili na sikuwahi kumuona akinitembelea tena.
“Guardiola ni rafiki na ningali namhitaji sana, lakini kusema ukweli hakuwa kule kwa ajili yangu. Ningependa kufanya mambo tofauti. Sitaki kusema lolote zaidi kuhusu hili,” alimaliza Vilanova kuungana na ukosoaji kuwa Guardiola hakumjali.
Jupp Heynckes
Heynckes agoma kumrithi Vilanova
KOCHA Jupp Heynckes (68) aliyempisha Pep Guardiola katika timu ya Bayern Munich baada ya kuipa mataji matatu msimu uliopita, amekataa kujiunga na Barcelona ya Hispania.
Ingawa amekuwa akitajwa katika orodha ya makocha wanaopewa nafasi ya kuinoa Barcelona, Heynckes amesema hana mpango wa kufundisha soka kwa sasa.
Alisema licha ya Barcelona kuondokewa na kocha wake Tito Vilanova ambaye amejiweka kando kwa matatizo ya kiafya, kocha huyo amesema anataka kufaidi matunda ya kazi aliyofanya kabla ya kustaafu.
Heynckes mwenye rekodi ya mafanikio makubwa katika ufundishaji wake, msimu uliopita ameiwezesha Bayern kutwaa mataji matatu.
Mataji hayo ni ubingwa wa Bundesliga,  Ligi ya Mabingwa Ulaya na Kombe la Ligi. Aidha, Heynckes amekuwa ni mwenye rekodi bora na michuano ya kimtaifa kwani mwaka 1998, aliipa Real Madrid ubingwa wa Ulaya.
“Nimekuwa ‘bize’ kwa muda mrefu, lakini sasa nimeamua kufanya kazi nyingine ya ufugaji na kutunza bustani, hivyo itakuwa vigumu kwangu kurejea kufundisha bada ya kuondoka Bayern Munich,” alisema alipozunguza na Sky Sport News na kuongeza:
“Natambua hisia za mwili wangu ambao mara nyingi umekuwa ukitamani kufundisha soka, lakini ni wakati sasa wa kubudika na matunda ya kazi niliyofanya kwa miaka mingi.
Hneyckes alitoa kauli hiyo baada ya kuulizwa kama yu tayari kuziba nafasi ya Vilanova ingawa baadhi ya makocha wamekuwa wakitajwa kama Gerardo Martino.
Kuna habari kuwa, Gerardo ndio chaguo la Lionel Messi, japo kuna majina mengine yanataja kwama Luis Enrique wa klabu ya Celta Vigo.
Enrique, 43, amekuwa mwenye mafanikio makubwa katika miaka mitatu hivi akiwa na kikosi cha pili cha Barcelona tangu mwaka 2008 na 2011 kabla ya kwenda AS Roma ambako hakupata mafanikio.
Naser Chadli
Spurs yanasa saini ya Chadli
KLABU ya Tottenham imethibitisha kumsajili nyota wa kimataifa wa Ubelgiji, Naser Chadli kutoka klabu ya  FC Twente kwa ajili ya msimu ujao.
Winga huyo mweye umri wa miaka 23, tayari jana alikuwa mjini hapa kukamilisha taratibu za kujiunga na klabu hiyo akifuata nyayo Wabelgiji wenzake, Mousa Dembele na Jan Vertonghen.
Chadli, anayecheza pia kama winga wa pembeni, ni mchezaji wa pili kusajiliwa Spurs akitanguliwa na  Mbrazil, Paulinho kutoka Corinthians aliyegharimu kiasi cha pauni mil 20.
Baada ya kukamilisha taratibu zote, ataungana na kikosi cha Kocha Andre Villas-Boas kilichopo Hong Kong kujiandaa na msimu mpya.
Reina na Benitez
Kipa Reina amfuata Benitez kwa mkopo
KOCHA wa Liverpool, Brendan Rodgers amesema kipa wa timu hiyo, Pepe Reina, atakwenda kwa mkopo katika klabu ya Napoli kutokana na sababu za kiuchumi.
Mipango hiyo inatokana na Napoli kutokuwa na uhakika wa kipa wake Julio Cesar ambaye hadi sasa hajaamua kuongeza mkataba.
Rodgers amesema Reina ataondoka Anfield msimu huu kwani Liverpool hawana uwezo wa kumlipa baada ya kutumia euro mil 10 kumsajili Simon Mignolet kutoka Sunderland, Juni mwaka huu.
Reina, aliyebakisha mkataba wa miaka mitatu ya kuicheza Liverpool, amekuwa akilipwa mshahara wa euro  128,000 kwa wiki, akiwa Napoli, atakuwa chini ya Rafa Benitez.
Benitez tayari amesajili nyota kadhaa kama kipa Rafael kutoka Santos kwa euro mil 5, lakini amekuwa akimhitaji Reina kuongeza ushindani wa namba.