Friday, August 16, 2013

Kanu: Nigeria Itatwaa Kombe la Dunia

Kanu: Nigeria Itatwaa Kombe la Dunia
Nwanko Kanu akiwa pamoja na familia yake.
MSHAMBULIAJI wa kimataifa wa zamani wa Nigeria, Nwankwo Kanu (37), amewatabiria mafanikio makubwa mabingwa wa Afrika, Super Eagles, kwamba wanaweza kuibeba Afrika katika kipute cha fainali za Kombe la Dunia za mwakani nchini Brazil.
Nwanko aliyewahi kuchezea kwa mafanikio makubwa katika klabu mbalimbali barani Ulaya ikiwemo Arsenal, amesema kwa ubora wa kikosi cha Super Eagles cha sasa na uwezo wa benchi la ufundi chini Stephen Keshi, timu hiyo itapata mafanikio makubwa katika fainali hizo.
“Tutacheza fainali za Kombe la Dunia mwakani tukiwa na shauku ya kubeba ubingwa kwa niaba ya Afrika. Na kuhusu mechi ya mwisho dhidi ya Malawi, tu tayari na tutashinda,” alisema Kanu alipozungumza na mtandao wa Goal na kuongeza: “Tuna kikosi bora cha ushindani kinachoweza kutupa raha katika fainali za Kombe la Dunia,” alisema Kanu.
“Tunahitaji wachezaji wenye njaa ya mafanikio na wenye uchungu na nchi wenye kutambua wajibu wao katika kuipigania nchi.
“Ndiyo sababu ya timu hii kufanya vizuri, japo uwepo wa nyota wazoefu ni sababu nyingine, wote hupambana kupigania ushindi.
“Nyuma ya wachezaji, tuna benchi lenye makocha bora walio tayari kuipa timu mafanikio,” alisema nyota huyo aliyekuwepo kwenye kikosi cha vijana wa chini ya miaka 23 kilichobeba medali ya dhahabu katika fainali za Olimpiki mwaka 1996.
Hata hivyo, ili Nigeria iweze kuvuka hatua ya makundi na kutinga hatua ya 10 bora itakayotoa timu tano za kwenda Brazil, inakabiliwa na mechi ya mwisho katika kundi F, dhidi ya Malawi itakayochezwa Septemba 6.
Katika mechi hiyo, Nigeria yenye pointi tisa, inahitaji walau sare tu kumaliza kinara wa kundi kutokana na Malawi chini ya Kocha wake Tom Saintfiet kuhitaji ushindi kwani itashuka dimbani
siku hiyo ikiwa na pointi saba.

Suarez, Liverpool wamaliza tofauti

Suarez, Liverpool wamaliza tofauti
HATIMAYE mshambuliaji wa kimataifa wa Uruguay, Luis Suarez, jana alifanya mazoezi na wenzake wa kikosi cha kwanza Cha Liverpool baada ya kufanya majadiliano na kocha wake, Brendan Rodgers.
Suarez, 26, aliyekuwa akitaka kuhama Anfield bila mafanikiuo, alirejea katika kikosi cha Liverpool tangu Alhamisi baada ya kuichezea Uruguay katika mechi ya kirafiki ya kimataifa dhidi ya Japan na kushindwa mabao 4-2, mjini Miyagi.

Awali, nyota huyo aliyekuwa akifanya mazoezi kivyake baada ya kutaka kulazimisha kuondoka Anfield kwa njia ya kisheria hadi pale atakapoomba radhi kwa kocha wake na klabu ya Liverpool.
Licha ya Suarez kuwindwa vikali na klabu kadhaa hasa Arsenal ambayo hata mchezaji mwenyewe alisema alitaka kujiunga nayo akitaka kucheza Ligi ya Mabingwa, mpango huo umekwama na nyota huyo amekubali matokeo.
"Ninataka kuelekeza nguvu na akili zangu katika kucheza soka," alisema Suarez atakayekosa mechi sita za Ligi Kuu inayoanza leo kwa kosa la kumng’ata sikio beki wa Chelsea, Branislav Ivanovic tangu Aprili mwaka huu.
Suarez, aliyetua Liverpool tangu Januari 2011, akitokea Ajax  ya Ufaransa kwa kitita cha pauni mil 22.7, amecheza jumla ya mechi 44 na kufunga mabao 30.

Ushabiki wamponza Mrisho Ngasa

Ushabiki wamponza Mrisho Ngasa
KAMATI ya Sheria na Hadhi za Wachezaji ya Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), imepitia usajili wa Ligi Kuu na kumuidhinisha mshambuliaji Mrisho Ngasa kuchezea timu ya Yanga, huku ikimfungia mechi sita na kumtaka kurejesha sh milioni 30 na fidia ya asilimia 50 kwa klabu ya Simba.
Kwa mujibu wa Ofisa Habari wa TFF, Boniface Wambura, kamati hiyo chini ya Mwenyekiti wake Alex Mgongolwa, imebaini kuwa ni kweli Ngasa alisaini mkataba mwingine Simba katika kipindi ambacho alikuwa na mkataba na Azam, ambako alipewa kiasi hicho cha fedha.
Kutokana na kubainika kwa hayo, Ngasa anatakiwa kurejesha fedha alizopokea, sh milioni 30, pamoja na fidia ya asilimia 50 (ambayo ni sh milioni 15), hivyo kulipa jumla ya sh milioni 45, kwa Wekundu wa Msimbazi, ambao walimtoa Azam FC kwa mkopo.
Kamati ya Mgongolwa, pia imemfungia Ngasa kucheza mechi sita za mashindano zilizo chini ya TFF, kuanzia Ngao ya Jamii kesho, baina ya Yanga na Azam FC, na anatakiwa awe amelipa fedha hizo ndani ya kipindi cha kukosa mechi hizo.
Endapo Ngasa atashindwa kulipa fedha hizo kwa wakati huo, hatoruhusiwa kucheza hadi atakapokamilisha hilo.
Aidha, kamati imepitia pingamizi zote zilizowasilishwa kuhusu usajili wa wachezaji, kukatiza mikataba na kuzitaka klabu husika ziwe zimetatua masuala hayo hadi Agosti 22.
Kwa upande wa wachezaji wa kigeni, kamati imeagiza wasiruhusiwe kucheza hadi watakapopata hati za uhamisho wa kimataifa (ITC), pamoja na vibali vya kufanya kazi nchini.
Kamati hiyo itakutana tena Agosti 23 ili kupata ripoti za pingamizi ilizoagiza ziwe zimefanyiwa kazi hadi Agosti 22 na kutoa uamuzi kwa pande ambazo hazikuafikiana.
Wakati huo huo, Kamati ya Uchaguzi ya TFF, kwa kuzingatia mamlaka iliyonayo katika kifungu cha 10(6), cha Kanuni za Uchaguzi, imesogeza mbele tarehe ya uchaguzi mkuu kutoka Oktoba 20 hadi 27, ukitanguliwa na mkutano mkuu siku moja kabla, huku ule wa Bodi ya Ligi Kuu ukibaki kuwa Oktoba 18.
Sababu za kusogeza mbele uchaguzi huo ni kutokana na kuwa Oktoba 20 uongozi wa TFF utakuwa na shughuli nyingi za maandalizi ya mechi ya Simba na Yanga na hivyo haitawezekana kusimamia shughuli za mkutano mkuu wa uchaguzi kwa wakati mmoja na mchezo huo.
Kutokana na mabadiliko hayo, siku ya mwisho ya kampeni itakuwa Oktoba 25, badala ya Oktoba 17 ya awali na ukiondoa mabadiliko hayo, ratiba ya mchakato wa uchaguzi itabaki kama ilivyotangazwa na kamati hiyo Agosti 24 mwaka huu.
Wambura alibainisha kuwa kamati inaamini wahusika wote watapokea vema mabadiliko yaliyotokana na Sekretarieti ya TFF kumwandikia Mwenyekiti wa Kamati ya Uchaguzi, kumuomba kupishanisha mechi na uchaguzi, kwa vile yeye na kamati yake ndio wenye mamlaka.