Monday, August 19, 2013

Simba yamtoa bure Shomari Kapombe

Simba yamtoa bure Shomari Kapombe

UONGOZI wa Simba, umemtoa bila ada beki wake mahiri Shomari Kapombe kwa klabu ya AS Cannes ya Ufaransa inayoshiriki Ligi Daraja la Nne kwa lengo la kumtafu timu kubwa ndani ya miaka miwili.
Usajili huo, haujawahi kutokea wala kufanywa na klabu yoyote ya Tanzania, ambako kwa makubaliano waliyoingia, Simba itakuja kupata gawio endapo tu atauzwa timu nyingine.
Kwa mujibu wa Ofisa Habari wa Simba, Ezekiel Kamwaga, ‘Mr Liverpool’ AS Cannes itamgharamia Kapombe kwa kila kitu wakati akiwa Ufaransa na lengo la mchezaji huyo kubaki huko ni kumfanya awe bora zaidi kuliko Asasa.
“Kwenye makubaliano hayo, Simba haitapata chochote kwa sasa. Isipokuwa endapo Kapombe atapata timu, Simba itapata mgawo wake kutoka katika mauzo hayo, makocha wa Ulaya wamebaini kwamba, Kapombe ni mchezaji mzuri lakini anahitaji kuboreshewa vitu vichache kabla hajawa mchezaji mkubwa wa kutumainiwa na klabu kubwa,” alisema Kamwaga.
 Alisema, katika mkataba huo mpya, Simba imeangalia zaidi maslahi ya Taifa na ya mchezaji kuliko ya klabu, kwa vile kama mchezaji huyo atapata nafasi Ulaya, hilo litafungua milango kwa wachezaji wengi wa Kitanzania, ambao kwa sasa hawapati fursa.
Wakala wa Kapombe, Denis Kadito, alisema, ingawa Kapombe ameonekana kuwa mchezaji mzuri, kutofahamika kwa jina la Tanzania kumekuwa kikwazo kikubwa kupata nafasi ya moja kwa moja na ndiyo maana imebidi aanzie kwenye hatua ya chini.
“Ofa hii ya Cannes ni nzuri, kwa sababu timu hiyo huwa inacheza na timu za akiba za klabu zote zinavyoshiriki katika Ligi Kuu ya Ufaransa na hivyo atakuwa anaonwa na mawakala wa timu kubwa kila wiki, hii itamsaidia kupata timu kubwa mapema ndani ya msimu mmoja kutoka sasa,” alisema Kadito.
Alisema, kutokana na mkataba huo wa Kapombe na Cannes, Simba sasa imeongeza mkataba wake na mchezaji huyo kwa miaka mitatu zaidi, kwa vile mkataba wake wa sasa unamalizika Aprili mwakani.
Aliongeza kuwa, Kapombe hatafanikiwa kupata timu katika kipindi cha miaka miwili kutoka sasa, atarejea klabu yake ya Simba kuendelea na majukumu yake.

Everton yakataa fedha za Man Utd

Everton yakataa fedha za Man Utd

KLABU ya Everton imeripotiwa kuikataa ofa ya pauni milioni 28 kutoka kwa Manchester United kwa ajili ya kuwasajili beki wa kushoto Leighton Baines na kiungo-mchezeshaji Marouane Fellaini.
Man United walituma ofa ya pauni milioni 16 kuomba ridhaa ya kumsajili Fellaini - wiki mbili baada ya kumalizika kwa muda wa kutengua kipengele chake cha kumuuza kwa ada ya pauni milioni 23.5, huku wakiongeza pauni 12 kwa ajili ya Baines.
Lakini katika namna ambayo haikutarajiwa, Everton haraka waliikataa ofa hiyo kutoka kwa kocha wao wa zamani David Moyes, ambaye kwa sasa anainoa Man United akirithi mikoba iliyoachwa wazi na Sir Alex Ferguson.
Inaaminika Everton watakuwa tayari kuwauza wachezaji hao kwa angalau kuanzia dau la pauni milioni 38 na sasa inasubiriwa kama Man United watakuwa tayari kuongeza paundi millioni 10 ili kufanikisha dili hilo kabla ya siku ya mwisho ya uhamisho wa kiangazi.
Harakati za Man United kumnasa Fellaini zinatokana na kukata tamaa ya kumpata Cesc Fabregas, huku Baines akija kuchukua mikoba ya Patrice Evra. Nyota wote wawili walikuwa kikosini katika mechi ya ufunguzi wa ligi ya sare ya 2-2 dhidi ya Norwich.
Moyes ni mfuasi mzuri wa soka la wakali hao, ambao wote aliwasajili akiwa Everton, Baines akimtoa Wigan kwa dau la pauni milioni 6 Agosti 2007, huku Fellaini akimng’oa Standard Liege ya Ubelgiji kwa dau rekodi ya klabu la pauni milioni 15, Septemba 2008.

Jose Mourinho ajifunga kitanzi Chelsea

Jose Mourinho ajifunga kitanzi Chelsea
SIKU moja baada ya ufunguzi wa msimu mpya wa Ligi Kuu ya hapa, kocha wa Chelsea, Jose Mourinho ameibuka na kuapa kwamba ataachana na jukumu lake klabuni Stamford Bridge kama hatoweza kutwaa mataji.
Mourinho, Mreno anayependa kujiita Special One, alitwaa mataji mawili ya Ligi Kuu ya Barclays katika kipindi chake cha kwanza kuinoa Blues na sasa amerejea kwa mara ya pili kuwanoa mabilionea hao wa Magharibi mwa jiji hili.
Lakini sasa, Mourinho anaahidi kujiweka kando katika jukumu la kuinoa Chelsea, kama ataendeleza ukame wa mataji ulioanzia Santiago Bernabeu yaliko makazi ya klabu ya Real Madrid, ambako alimaliza msimu uliopita bila kikombe.
"Bila shaka, katika suala la kutwaa mataji. Hakuna mabadiliko katika DNA yangu, sijabadilika chochote pia katika asili yangu," alisema kuwaambia wanahabari wakati wa maandalizi ya mwisho kuelekea mechi yao ya jana.
Mourinho aliongeza: "Mimi si aina ya mtu ninayeweza kukaa katika klabu moja kwa misimu mitatu au minne bila kutwaa taji lolote.
"Katika hilo, mimi sihitaji klabu kuniambia 'hatuna furaha kuwa na wewe, kwaheri'.
"Mimi nitakuwa wa kwanza kusema 'nimejitoa kwa kila nilichoweza, lakini sijapata mafanikio, hivyo acha kila mmoja baina yetu awe kivyake na kujaribu mambo kivingine'," alijinasibu Mourinho.

25 wachukua fomu Uchaguzi Mkuu TFF

25 wachukua fomu Uchaguzi Mkuu TFF
WAGOMBEA 25 wamejitokeza kuchukua fomu za kuwania nafasi mbalimbali za uongozi katika uchaguzi wa Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), unaotarajiwa kufanyika Oktoba 27.
Kwa mujibu wa Ofisa Habari wa TFF, Boniface Wambura, fomu hizo zilianza kutolewa Agosti 16 na hadi jana, wagombea wawili wamejitosa nafasi ya rais, ambao ni Jamal Malinzi na Omar Nkwarulo huku Makamu wa Rais ni Ramadhani Nasib na Wallace Karia.

Aliwataja waliochukua fomu za kuwania ujumbe kuwa ni Athumani Kambi, Charles Komba, Davis Mosha, Elias Mwanjala, Eliud Mvella ‘Wamahanji’, Epaphra Swai, Farid Nahdi, Hussein Mwamba, Jumbe Magati, Kamwanga Tambwe na Khalid Mohamed.
Wengine ni Muhsin Balhabou, Omari Abdulkadir, Omari Walii, Samwel Nyalla, Shaffih Dauda, Stanley Lugenge, Twahir Njoki, Vedastus Lufano, Venance Mwamoto na Wilfred Kidau.
Kwa upande wa Bodi ya Ligi Kuu, aliyechukua fomu ni Hamad Yahya anayewania uenyekiti.

Messi: Msinigombanishe na Ronaldo

Messi: Msinigombanishe na Ronaldo
MSHAMBULIAJI wa FC Barcelona, Lionel Messi amekanusha dhana iliyoshamiri miongoni mwa mashabiki wa soka duniani kuwa yeye na nyota wa Real Madrid, Cristiano Ronaldo wana chuki na uhasama.
Wakali hao wamekuwa katika vita ya kuwania tuzo za soka duniani, ambapo Messi, alikiri kuvutiwa na soka la mpinzani wake huyo, huku akifafanua kuwa anafanya kazi yake kwa faida ya klabu na si kumthibitishia Ronaldo kuwa yeye ni zaidi.
"Hakuna chuki binafsi (na Ronaldo) kwa namna yoyote," alisema Messi Mwanasoka Bora wa Mwaka wa Fifa mwenye miaka 26 kuliambia gazeti la Maxim.
"Ronaldo ni mtu mzuri na anaweza kubadili mchezo wowote. Yeye anafanya vitu kivyake na mimi najitoa kadiri niwezavyo kuipa mafanikio Barcelona," alisisitiza Messi nyota wa kimataifa wa Argentina.
Messi alikuwa akisisitiza nia yake ya kufikia malengo binafsi, lakini muhimu zaidi ni kufanikisha mipango ya klabu yake, hasa katika kipindi hiki ambacho inajaribu kuzika jinamizi la kujiondoa kazini kwa kocha wao Tito Vilanova.
"Tunataka kutwaa ubingwa wa Hispania na Ulaya msimu huu," alifichua na kuongeza: "Ilikuwa ni huzuni kwa namna Vilanova alivyoondoka, lakini kwa sasa sote tuko chini ya kocha mpya (Tata Martino).
"Na sio suala la bahati mbaya kwamba wachezaji wa Barcelona tumekuwa tukifanya masuala ya kimaisha chini na kutupa mafanikio.
"Tunajitambua kwamba sisi ni wachezaji, sio nyota wa filamu. Wakati tusipokuwa na mazoezi au mechi, tunakuwa nyumbani na familia zetu," alisema Messi.

Mgongolwa amemuangushi jumba bovu Mrisho Ngasa

Mgongolwa amemuangushia 
jumba bovu Mrisho Ngasa

NIMESHANGAZWA na uamuzi wa Kamati ya Sheria na Hadhi za wachezaji juu ya mchezaji Mrisho Ngasa. Kwamba kamati hiyo imemfungia kucheza mechi sita za mashindano yanayosimamiwa na Shirikisho la Soka Tanzania (TFF) na kumuamuru kurejesha fedha za klabu ya Simba Sh. milioni 30 na fidia ya asilimia 50 ya fedha hizo, kufanya jumla ya Sh. 45 milioni anazotakiwa kuilipa Simba.
Mwenyekiti wa kamati hiyo mwanasheria Alex Mgongolwa amesema wametoa adhabu hiyo dhidi ya Ngasa kwa sababu wamebaini mchezaji huyo aliyesajiliwa na Yanga, alikuwa ameingia mkataba mwingine na Simba wakati akiichezea timu hiyo kwa mkopo akitokea timu ya Azam ambayo alikuwa na mkataba nayo uliomalizika Mei 31, mwaka huu.
Uamuzi huu ni wa kushangaza sana. Ninashindwa kuelewa kama kamati hii ilifikia uamuzi huu kwa kuongozwa na sheria. Kwanza, hicho kinachodaiwa kuwa mkataba kati ya Ngasa na Simba hakina nguvu ya kisheria ya kuitwa mkataba, hivyo hakikuwa na hadhi ya kujadiliwa na kamati hiyo.
Nasema makubaliano kati ya Ngasa na Simba hayakuwa na nguvu ya kisheria kwa sababu ili makubaliano kati ya mchezaji na klabu yakamilike kuwa nyaraka ya kisheria ni lazima makubaliano hayo yasajiliwe na TFF.
Makubaliano kati ya Ngasa na Simba hayakusajiliwa na TFF,  hivyo hayawezi kuwa mkataba wa kisheria kwa mujibu wa kanuni za TFF na hivyo hayawezi kujadiliwa na Kamati ya Mgongolwa (Rejea sakata la Mbuyu Twite  na Simba).
Pili, makubaliano kati ya Ngasa na Simba hayana nguvu za kisheria kwasababu wakati Ngasa akisaini makubaliano hayo na Simba, tayari alikuwa na mkataba mwingine na Azam ambao ulikuwa katika makabati ya TFF.
Kwahiyo, kisheria mkataba unaotambulika ni ule wa kwanza kati ya Ngasa na Azam. Kwanini leo kamati ya Mgongolwa iseme Ngasa alikuwa ameingia mkataba na Simba ilihali yale yalikuwa makaratasi tu yasiyo na maana yoyote?
Kamati ya Mgongolwa haikupaswa kujadili suala hili na kulitolea maamuzi. Hayo yalikuwa makubaliano ya kihuni yaliyofanyika uchochoroni, hivyo Kamati ya Mgongolwa ingewaambia Simba na Ngasa waende wakamalizane huko huko uchochoroni.
Hata kama makubaliano hayo yanachukuliwa kuwa mkataba halali, basi haliwezi kuwa kosa la Ngasa pekee yake. Wote wawili, mchezaji na klabu ya Simba wana makosa kwa mujibu wa kanuni za Fifa.
 Kosa la Simba ni kufanya mazungumzo na kuingia mkataba na mchezaji wa timu nyingine bila klabu inayommiliki kuwa na taarifa. Kwanini leo Ngasa aadhibiwe pekee yake? Wote walipaswa kuadhibiwa. Chelsea na mchezaji Ashley Cole waliwahi kuadhibiwa baada ya kubainika kufanya mazungumzo bila kibali cha timu ya Arsenal iliyokuwa ikimmiliki mchezaji huyo.
Halafu Kamati ya Mgongolwa imemhukumu Ngasa kukosa mechi sita, kwa kosa gani hasa? Ni kanuni ipi ya TFF au Fifa iliyowaongoza kufikia adhabu hiyo? Ngasa na Simba walipaswa kuhukumiwa kulipa faini kwa kosa la kufanya mazungumzo na kuingia mkataba bila kibali cha Azam.
Kitu kingine kinachozusha maswali na kutia shaka uhalali wake ni adhabu aliyopewa Ngasa na Kamati ya Mgongolwa ya kutakiwa kulipa fidia ya asilimia 50 ya fedha alizopewa na Simba Sh. milioni 30. Fidia ya asilimia 50 ipo kisheria? Suala la riba linaongozwa na sheria za fedha za Benki Kuu na siyo suala la kuamua tu unavyotaka.
Isitoshe, adhabu hii inayapa nguvu za kisheria makubaliano ya Simba na Ngasa na kuyafanya kuwa mkataba halali wa kisheria, na hivyo kumfanya Ngasa aonekane amesaini
timu mbili, Simba na Yanga. Kwanini sasa Kamati ya Mgongolwa imuidhinishe kuchezea Yanga wakati alianza kusaini Simba? Huu ni uamuzi wa fedheha kwa kosa letu.