Friday, August 23, 2013

Raul arudi Santiago Bernabeu,
afunga bao na jezi ya Cristiano

NYOTA wa zamani wa Real Madrid, Raul Gonzalez, jana usiku alirejea Santiago Bernabeu akivalia jezi yake No 7, aliyokuwa akivalia kabla ya kutimkia Al Saad ya Qatar, ambayo sasa inavaliwa na Cristiano Ronaldo.
Raul alipata fursa ya kuvalia jezi hiyo katika mechi ya kirafiki baina ya timu hizo mbili ambapo alichezea timu zote mbili, dakika 45 kila moja na kuifungia Real Madrid bao dhidi ya timu yake ya sasa, Al Saad.
Katika mechi hiyo ya aina yake ya kuwania kombe la Santiago Bernabeu, Raul mwenye umri wa miaka 36, alionesha kiwango bora huku akibubujikwa na machozi, baada ya filimbi ya mwisho.
Akiwa kwenye jezi namba 7, Raul aliwapungia na kuukisi umati baada ya kuifungia bao Real Madrid kutokana na pasi nzuri ya Angel Di Maria.
Kabla ya kuanza kwa mechi hiyo, Raul alipata mapokezi ya aina yake kutokana na kuifanyia makubwa timu hiyo kabla hajaondoka huku akipewa mshipi wa unahodha na kipa, Iker Casillas.
Wakati wa mapumziko, Raul akiwa na jezi na 7, alikimbia hadi kwa mmiliki wa jezi hiyo kwa sasa, Cristiano Ronaldo, ambaye katika kipindi cha kwanza katika mechi hiyo, alivalia jezi namba 11.
Walipokutana, wawili hao walikumbatiana kwa furaha na kuzungumza machache kabla ya Raul kwenda kuvalia jezi ya Al-Saad kwa kipindi cha pili.
Hata hivyo, mechi hiyo iliisha vijana wa Carlo Ancelotti kuiwezesha Real Madrid kutwaa Kombe la Santiago Bernabeu mara ya tisa mfululizo kwa ushindi wa mabao 5-0.
Mabao ya wenyeji yalifungwa na Isco goal, Benzema aliyefunga kwa penalti huku Jese akifunga mawili.
Raul alitimkia Qatar mwaka 2012, baada ya kucheza misimu miwili katika klabu ya Schalke ya Ujerumani.
Mashabiki wa Real Madrid wamekuwa wakimheshimu Raul kutokana na  mchango wake mkubwa, akiongoza kwa ufungaji wa mabao, akicheka na
nyavu mara 323 katika mechi 741.

No comments:

Post a Comment