Tuesday, July 23, 2013

Safari ya Azam ‘Sauzi’ yaiva
SHIRIKISHO la soka Tanzania (TFF) limebariki ziara ya Azam FC (pichani) nchini Afrika Kusini kujifua kwa wiki mbili kabla ya kurejea tayari kwa msimu mpya wa Ligi Kuu itakayoanza Agosti 24.
Kwa mujibu wa Katibu Mkuu wa Klabu hiyo, Idrisa Nassoro, Azam itakayoondoka Agosti 2, itacheza mechi tatu za kirafiki ambapo baada ya kurejea itacheza mechi ya Ngao ya Hisani Agosti 17, ikiwa ni ufunguzi wa msimu mpya. 
Nassoro alisema, maandalizi ya safari hiyo yamekamilika kwani wachezaji wote wapo tayari isipokuwa wachezaji wawili Brian Umonyi na Anfrey Mieno ambao watabaki kutokana na kuwa majeruhi.
“Kila kitu kimekamilika tumebakia kuondoka tu, TFF wana taarifa juu ya safari yetu. Umonyi anasumbuliwa na maumivu ya msuli huku Mieno akiwa na maumivu ya kifundo cha mguu,” alisema Nassoro.
Alisema kukawia kwa safari yao ilikuwa ni kusubiri uhakika wa tarehe ya kuanza kwa Ligi Kuu pia baadhi ya nyota wao kuwemo kwenye kikosi cha timu ya soka ya Tanzania, Taifa Stars inayokabiliwa na mechi dhidi ya Uganda itakayochezwa mwishoni mwa wiki hii mjini Kampala.
Akizungumzia ziara hiyo, Katibu Mkuu wa TFF, Angetile Osiah alikiri kupata barua ya ziara ya Azam na kuwatakia kila la kheri katika ziara hiyo kujiandaa na msimu mpya wa Ligi Kuu.
Mbali ya Ligi Kuu ya Bara, Azam chini ya Kocha wake Stewart Hall, inakabiliwa na michuano ya Kombe la Shirikisho kama ilivyokuwa msimu uliopita ambapo licha ya kucheza mara ya kwanza, ilifika hadi raundi ya pili iking’olewa na FAR Rabat ya Morocco.  

No comments:

Post a Comment