Tuesday, July 23, 2013

Kim ahofia saumu Stars
KOCHA Mkuu wa timu ya soka ya Tanzani, Taifa Stars, Kim Poulsen amesema vijana wake wameiva kuwakabili Uganda kwenye mechi ya marudiano ya mchujo kuwania tiketi ya Fainali za Kombe la Afrika kwa Wachezaji wa Ndani (CHAN) itakayochezwa Jumamosi, jijini Kampala.
Akizungumza na waandishi wa habari jijini Mwanza jana, Kim amesema tangu kikosi chake kimeingia kambini Julai 14, wachezaji wamekuwa wakifanya vizuri kwenye mazoezi na wako tayari kwa mechi hiyo.
“Uganda ni timu bora kwa ukanda huu wa Afrika Mashariki na Kati. Mechi itakuwa ngumu, tunaamini tunakwenda kufanya vizuri. Tayari tunayo mikakati kwa ajili ya mechi hiyo, tunakwenda kuikamilisha Kampala,” alisema Kim.
Hata hivyo, Kim amesema licha ya mwitikio mzuri wa wachezaji kwenye mazoez,  lakini wanakabiliwa na changamoto ya wengi wao kuwa wamefunga wakati wachezaji wanapokuwa kambini wanatakiwa kula, kunywa na kupumzika.
“Hiki ni kipindi kigumu kisoka, suala la kufunga ni la kiimani ambapo hatuwezi kuwazuia wachezaji kufunga. Karibu nusu ya wachezaji wanafunga, hii ni changamoto ambayo tunaiheshimu,” amesema Kim na kuongeza ni wazi kikosi chake cha kwanza kitakuwa na mabadiliko baada ya beki Shomari Kapombe kwenda kwenye majaribio nchini Uholanzi.
Stars inayodhaminiwa na Kilimanjaro Premium Lager inaondoka Mwanza leo saa 7.25 mchana kwa ndege ya PrecisionAir na kuwasili Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Entebbe saa 8.15 mchana.
Nyota waliomo kwenye msafara huo ni makipa Juma Kaseja, Mwadini Ali na Ali Mustafa. Mabeki ni Aggrey Morris, David Luhende, Erasto Nyoni, Kelvin Yondani, Nadir Haroub na Vincent Barnabas.
Viungo ni Amri Kiemba, Athuman Idd, Frank Domayo, Haruni Chanongo, Khamis Mcha, Mudhathir Yahya, Salum Abubakar na Simon Msuva. Washambuliaji ni John Boko, Juma Luizio na Mrisho Ngasa.
Stars inakwenda Uganda ikiwa nyuma kwa bao 1-0 walilofungwa katika mechi ya kwanza iliyochezwa Julai 13, kwenye Uwanja wa Taifa, jijini Dar es Salaam Julai 13; huku mshindi wa jumla baina yao atajitwalia tiketi ya kwenda Afrika Kusini kwa fainali za mwakani.

No comments:

Post a Comment