Wednesday, July 24, 2013

Kazimoto arejea kimiujiza
HATIMAYE kiungo wa Simba, Mwinyi Kazimoto, aliyetimkia nchini Qatar amerejea jijini Dar es Salaam kimya kimya huku uongozi wa klabu yake ukiwa haufahamu kuhusu ujio wake.
Kazimoto alitoweka bila taarifa akiwa timu ya taifa ‘Taifa Stars’ baada ya kumalizika kwa mchezo wa awali dhidi ya Uganda, uliomalizika kwa Stars kulala bao 1-0 na nafasi yake kuwa matatani.
Kutokana na kitendo chake hicho, nafasi yake timu ya taifa ilizibwa na Mudathir Yahya wa Azam FC.
Habari ilizozipata Tanzania Daima jana kutoka kwa mtu wa karibu na Kazimoto, zilisema kuwa alionekana eneo la Kinondoni Moscow usiku wa juzi akiwa na baadhi ya wachezaji wa moja ya timu za Ligi Kuu Tanzania Bara inayomilikiwa na moja ya majeshi ya hapa nchini.
“Mnahangaika kumtafuta na kujiuliza Kazimoto yuko wapi, mimi nimemuona jana Kinondoni kwa macho yangu akiwa na wachezaji wa ... ila alikuwa kweli nje ya nchi na amerudi,” alisema mtoa habari huyo.
Aidha, chanzo hicho kilienda mbali na kubainisha kuwa kiungo huyo ameshindwa kufuzu alikokuwa ndiyo sababu ya kurejea kimya kimya bila ya kuutaarifu uongozi.
Baada ya kurejea, Kazimoto anatarajiwa kukumbana na adhabu kutoka Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), kutokana na utovu wa nidhamu aliouonesha, huku pia klabu yake nayo ikitarajiwa kumpa adhabu pia.
Katibu Mkuu wa TFF, Angetile Osiah, alikaririwa hivi karibuni kuwa, Kiungo huyo endapo atapatikana atapewa adhabu kutokana na kanuni ambazo alisaini wakati akiingia kambini zinavyosema.
Kwa upande wa Simba, Katibu wake Mkuu, Evodius Mtawala, alikiri kusikia taarifa hizo na kudai kuwa wanamsubiri arejee kundini, kwa kuwa ana mkataba na klabu hiyo.
“Tumesikia tu, ila bado hatujamuona, tunamsubiri akija mwenyewe klabuni ndipo tutajua jinsi ya kumwadhibu, kwani aliondoka bila ya kututaarifu,” alisema Mtawala.

No comments:

Post a Comment