Tuesday, July 30, 2013

Fabregas: Sing’oki Barcelona
BARCELONA waliionya Manchester United chini ya kocha David Moyes kuwa wanapoteza muda katika jaribio la kumng’oa Cesc Fabregas Nou Camp kwenda Old Trafford na sasa imedhihirika hivyo.
Kiungo huyo wa kimataifa wa Hispania, amewaambia marafiki zake wa karibu kuwa yu tayari kwa vita ya kugombea namba na kujihakikishia nafasi katika kikosi cha Barca.
Manchester United tayari ilikwishatoa ofa mbili na zote zikakataliwa na Barcelona, kabla ya sasa kuratibu ofa ya tatu ya pauni milioni 35 ambayo itakuwa rekodi ya klabu.
Fabregas, 26, bado anaongoza orodha ya wakali wanaowindwa na Moyes kiangazi hiki, lakini chanzo cha ndani klabuni Nou Camp kimethibitisha juzi usiku: “Cesc amesifia mno ofa za Man United na anatambua nini thamani ya ofa zao kwake.
“Lakini ni miaka miwili tu tangu alipoondoka England alikokuwa akiichezea Arsenal na hatarajii kuihama tena Barcelona hususan hivi karibuni.
“Amekuwa katika vita akijaribu kuchuana na Xavi Hernandez na Andres Iniesta, ili kufanikiwa kupangwa upande wa pili baada yao, lakini yeye ameshiriki sehemu ya michezo yao na anahitaji nafasi zaidi ya hiyo,” kilifichua chanzo hicho.
Na kocha mpya Barca, Tata Martino, ambaye amechukua mikoba iliyoachwa wazi na Tito Vilanova aliyebwaga manyanga ili kujiuguza kansa ya tezi, amesisitiza kuwa atomruhusu kijana wake huyo kwenda popote.
Martino alisema: “Man United wanamtaka Cesc? Kama wamekataliwa ofa zao mbili za kumpata, watambue kuwa nitakataa na ofa yao ya tatu pia. Cesc atakuwa nasi hapa,” alisisitiza Martino raia wa Argentina.
Fabregas juzi aliripotiwa kuungana na wenzake katika kambi ya kujiandaa na msimu mpya na alifanyiwa vipimo vya afya kabla ya msimu kisha kujumuika na wenzake.

No comments:

Post a Comment