Wednesday, July 31, 2013

Klabu 10 zasusia uchaguzi SLFA
KLABU 10 miongoni mwa 14 za Ligi Kuu ya soka ya nchini hapa, zimegomea ligi hiyo kupinga kitendo cha Mohamed Kallon na wengine wanne kuchujwa kwenye mbio za uchaguzi wa Chama cha Soka (SLFA).
Tayari klabu hizo zimeandika barua ya kutoshiriki ligi hiyo na kuikabidhi kwa Bodi ya Ligi Kuu kutohusishwa kwenye ratiba ya ligi hiyo iliyokuwa itolewe hivi karibuni kwamba Kallon na wenzake wamechujwa kimizengwe.
Kalabu hizo zilizogomea ligi hiyo ni Diamond Stars, Gem Stars, Kambui Eagles, Old Edwardians FC, FC Kallon, Bo Rangers, Ports Authority FC, Mighty Blackpool, Central Parade FC na Freetown City FC.
Wakati hizo zikigoma, nyingine nne zilikuwa tayari kuendelea na ligi hiyo iliyokuwa ianze Jumatatu ijayo kwa mechi kati ya Bo Rangers na Mighty Blackpool.
Kallon, nyota wa zamani wa Inter Milan ya Italia na AS Monaco ya Ufaransa, alichujwa kwenye mbio hizo kwa kile kilichoelezwa kutokidhi vigezo kwa mujibu wa Ibara ya 32 (4) ya Katiba ya SLFA.
Kipengele hicho kinataka mgombea katika uchaguzi huo awe ni mkazi wa Sierra Leone si chini ya miaka mitano, kigezo ambacho kinamtupa nje Kallon ambaye anasema ni siasa za soka.
Wagombea wengine waliochujwa kwa nafasi ya rais wa chama hicho ni Rodney Michael na Foday Turay ambao ni kutokana na kutokidhi matakwa ya katiba hiyo ibara ya 25, inayohusu maadili kwa upande wa shughuli za kamari.
Hata hivyo, wagombea hao wamepinga kuchujwa kwao kwa hoja kuwa imetafsiriwa isivyo na kamati iliyowachuja, hivyo wanataka majina yao yarejeshwe kwenye kipute hicho.
Mashabiki wa Kallon na Michael wameitisha maandamano ya amani kuelekea Ikulu mjini hapa Jumatatu kutaka wagombea hao warejeshwe katika uchaguzi huo wa Agosti 3.
Rais wa Sierra Leone, Ernest Bai Koroma, amekutana na  Kallon na wafuasi wake na kuahidi kulishughulikia suala hilo kwa masilahi ya soka ya nchini hapa.
Kallon, nahodha wa zamani wa timu ya taifa, Leone Stars, ameiambia BBC kuwa anaamini Rais Koroma atamaliza mgogoro huo.
Wengine waliochujwa katika uchaguzi huo katika nafasi nyingine ni Idrissa Taralley na John Dissa kutokana na kuhusika kwao na shughuli za uendeshaji wa kamari.
Uchaguzi huo uliopangwa kufanyika Jumamosi chini ya Kamati ya Maridhiaano, ni baada ya kuahirishwa mara kadhaa kabla ya Shirikisho la Soka la Kimataifa (Fifa), kuingilia kati Desemba mwaka jana.
Kuchujwa kwa Kallon na wengine kunatoa nafasi kwa mgombea, Isha Johansen, kushinda kirahisi nafasi ya urais kutokana na kukosa mpinzani.

No comments:

Post a Comment