Monday, July 29, 2013

Kipigo cha Stars chagusa wadau
Wachezaji wa Uganda wakishangili moja ya bao walipokutana na Stars
SIKU moja baada ya timu ya soka ya Tanzania, Taifa Stars kuikosa tiketi ya kucheza fainali za Afrika kwa nyota wa ligi za ndani (CHAN) kwa kufungwa na Uganda mabao 4-1, wadau wamekuwa na maoni tofauti juu ya sababu ya kufungwa na nini kifanyike.
Kwa kipigo hicho, Stars chini ya kocha wake Kim Polsen imeshindwa kwenda nchini Afrika Kusini ambako kutachezwa fainali hizo mapema mwakani, ikiwe ni pigo jingine kwa tiumu hiyo baada ya kukosa tiketi ya Kombe la Dunia, pia mwakani nchini Brazil.
Ally Hassan Msumari ametoa lawama kwa Shirikisho la soka Tanzania (TFF) akisema limekuwa sehemu ya kushindwa huko kwa kushindwa kuiandaa vizuri timu hiyo ambayo wadau waliipa nafasi ya kwenda Afrika Kusini.
Alisema tatizo jingine la timu hiyo ni benchi la ufundi kuwakumbatia baadhi ya wachezaji licha ya kutokuwa na uwezo mkubwa kutokana na kuchoka na kupendekeza mabadiliko katika benchi la ufundi.
Naye Magige Flaviani alihoji uwezo wa Kim akisema ni wakati wa kuachia ngazi kuwapisha wengine wenye uwezo wa kuipatia timu hiyo mafanikio zaidi kwani tayari ilishaanza kupendwa na wengi.
Ally Hoza kwa upande wake alisema sababu ya kufungwa kwa Stars katika mechi zote mbili dhidi ya Uganda, ni wachezaji kuzidiwa kutokana na aina ya maandalizi waliyopewa.
Maoni hayo ya wadau yamekuja huku wachezaji wa Stars inayodhaminiwa na Kampuni ya Bia Tanzania (TBL) kupitia bia yake ya Kilimanjaro Premium Larger, wakipewa matunzo bora zaidi ikilinganisha na ilivyokuwa zamani.
Msafara wa timu hiyo ulitarajiwa kurejea nchini jana usiku majira ya saa 4 huku kocha wake (Kim) akisema wamekubali matokeo na kilichobaki ni kujipanga kwa kampeni zijazo.

No comments:

Post a Comment