Monday, October 14, 2013

Mkongwe Van der Sar amfagilia De Gea

Mkongwe Van der Sar amfagilia De Gea
KIPA wa zamani wa Manchester United, Edwin van der Sar amemsifu kipa namba moja wa timu hiyo, David de Gea, akisema ni miongoni mwa nyota ambao wataisaidia timu hiyo kutetea ubingwa wa Ligi Kuu msimu huu.
De Gea ni kipa aliyeonesha uwezo mkubwa langoni tangu kuanza kwa msimu huu ikiwemo katika mechi dhidi ya Sunderland walipotoka nyuma na kushinda 2-1.
Wakicheza nyumbani, Sunderland walitangulia kupata bao dakika ya tano likipachikwa wavuni na Emanuele Giaccherini kabla ya Januzaj kufunga mawili dakika za 55 na 61.
Katika mechi hiyo, mrithi huyo wa Van Der Sar, aliyetua Old Traffod kwa dau kubwa wakati huo akiwa na umri wa miaka 20, alionesha uwezo mkubwa langoni.
"Huwezi kuamini," alisema kipa huyo wa zamani wa Man Utd, ambaye sasa ni Meneja Masoko wa klabu ya Ajax ya Uholanzi na kuongeza kuwa, ameweza kucheza ligi tofauti akiwa na umri mdogo.
"Alitua Old Trafford kutokea Hispania akiwa hawezi kuzungumza kiingereza na kula chakula tofauti, mbinu tofauti na mazoezi tofauti, lakini ameweza kukabiliana nayo.
"Upigaji wa soka ya England katika kona na adhabu ya nje na ndani ya boksi, ni tofauti kabisa na Hispania, kwa vyovyote alipata ugumu kuzoea katika siku za awali,” alisema akimfagilia kipa huyo.
Alisema kwa vile bado ni kijana mdogo, kipa huyo ataopata mafanikio makubwa katika maisha yake ya soka kwani kwa kipindi alichodumu Old Trafford, atakuwa amejifunza mengi."